Share this to

By:Robert Mutasi

Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo imeitaka Bunge kuharakisha kupitishwa kwa miswada muhimu ya kilimo na marekebisho yake, ikisema hatua hiyo ni ya msingi katika kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza uzalishaji na kulinda maslahi ya wakulima nchini.

Waziri wa Kilimo, Mutahi Kagwe, ameonya kuwa kushindwa kupitisha miswada hiyo kabla ya mwezi Desemba kutahatarisha utekelezaji wa mageuzi yaliyopangwa katika sekta ya kilimo kutokana na muda wa kisheria unaokaribia kuisha.

“Kwa upande wetu mwezi Desemba. Kama hatuna chochote, kama tunataka mambo yapitishwe na Bunge katika kipindi hiki cha Bunge na hatujaiandaa ifikapo Desemba, haitatokea. Kwa hivyo ni muhimu sana na hapa ndipo nataka kutoa wito maalum kwa wanakamati wetu tafadhali saidieni miswada tuliyonayo huko, marekebisho tuliyonayo huko, lazima tuyakamilishe kati ya sasa na Desemba,” alisema Kagwe.

Akizungumza wakati wa kikao cha mashauriano kati ya Wizara na kamati za Bunge, Kagwe alisema miswada hiyo inalenga kutatua changamoto za muda mrefu zinazoikabili sekta ya kilimo, zikiwemo kuongeza uzalishaji wa mazao, kuimarisha usalama wa chakula, kuboresha masoko na kuhakikisha wakulima wanapata thamani stahiki ya mazao yao.

Wizara imeeleza kuwa tayari imeandaa ratiba ya kuwasilisha miswada hiyo Bungeni, lakini imehimiza ushirikiano wa karibu kutoka kwa kamati husika ili kuhakikisha mchakato unakamilika kabla ya muda uliowekwa. Kagwe alisisitiza kuwa bila mfumo imara wa kisheria, juhudi za Serikali za kutekeleza mageuzi ya sekta ya kilimo na kuafiki Ajenda ya Mageuzi ya Kiuchumi ya Chini kwenda Juu (BETA) zitakumbwa na changamoto.

Miswada hiyo inahusu maeneo mbalimbali ya sekta ya kilimo, ikiwemo mazao, mifugo, usalama wa chakula, malisho, udhibiti wa shughuli za kilimo na usimamizi wa mazao baada ya mavuno. Pia inalenga kuweka mfumo wa kisasa wa kisheria, kukuza kilimo kinachostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha taasisi zinazowahudumia wakulima.

Aidha, Wizara imeitaka Bunge kuhakikisha kunakuwa na ushirikishwaji mpana wa umma na wadau mbalimbali ili sheria zitakazopitishwa ziakisi mahitaji halisi ya wakulima, hasa wakulima wadogo ambao ndio uti wa mgongo wa uzalishaji wa chakula nchini.

Wito wa Kagwe unajiri wakati Kenya inaendelea kukabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi, huku mvua zinazotarajiwa za El Niño zikihofiwa kuathiri uzalishaji wa mazao muhimu kama mahindi, ngano, shayiri na mazao ya bustani. Wizara pia inataka sheria zitakazorahisisha usimamizi wa mazao baada ya mavuno, mfumo wa stakabadhi za ghala na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika kilimo.

Viongozi wa Bunge waliohudhuria kikao hicho wameahidi kushirikiana na Wizara ili kuharakisha mchakato wa kupitisha miswada hiyo, wakisisitiza kuwa sekta ya kilimo inaendelea kuwa mhimili mkuu wa uchumi wa Kenya na chanzo kikuu cha ajira kwa mamilioni ya wananchi.

Kagwe ameonyesha matumaini kuwa kupitia ushirikiano kati ya Serikali na Bunge, miswada hiyo itapitishwa kwa wakati na kuweka msingi wa sekta ya kilimo yenye ushindani, tija na uwezo wa kukabiliana na changamoto za siku zijazo.

Katika miezi ya hivi karibuni, Wizara imekuwa ikiendesha mikutano ya ushirikishwaji wa umma katika maeneo mbalimbali nchini ili kukusanya maoni ya wadau kuhusu miswada hiyo kabla ya kuwasilishwa rasmi Bungeni.


Share this to

By admin

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *